Wakazi wa Singida mashabiki wa Singida Black Stars na wapenzi wa mpira wa miguu wameonyesha kufurahishwa na ujenzi wa uwanja mpya wa Singida Black Stars uliozinduliwa rasmi na naibu Waziri wa Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo Hamisi Mwinjuma huku wakizinyooshea kidole klabu kongwe nchini za Simba na Yanga
Wakizungumza katika nyakati tofauti uwanjani hapo mara baada ya ufunguzi wamesema uzinduzi wa uwanja huo iwe somo kwa timu kubwa nchini kutokana na Singida kuwa timu changa lakini imeweza kujenga na kumiliki uwanja wake huku timu kubwa zimeshindwa kufanya hivyo licha ya ukongwe wake
Kwa mujibu wa mjumbe wa bodi ya Singida Black Stars ambaye pia ni mbunge wa Makete Festo Sanga amesema uzinduzi huo ni awamu ya kwanza (Phrase one) ambayo ni eneo la kuchezea lililokamilika kwa asilimia 100 huku awamu ya pili ikiwa ni ujenzi wa majukwaa ya watazamaji
Ametumia nafasi hiyo kuwaita wadau kuwaunga mkono na
kuwekeza kwenye ujenzi unaondelea hususani majukwaa na maeneo mengine ili
kufanikisha uwanja huo kuwa bora kama ambavyo umekusudiwa mara baada ya
kukamilika kwake
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Hamisi Mwinjuma amesema kujengwa kwa uwanja huo kunaonyesha nia ya dhati ya ukuaji wa klabu hio changa huku akiwataka Singida Black Stars kuhakikisha wanapata matokeo na sio kuziacha timu kubwa za simba na yanga pekee
Uwanja huo uliojengwa eneo la Mtipa katika Manispaa ya
Singida mkoani hapa, umepewa jina la AIRTEL STADIUM na rasmi Singida Black Stars
watahama kutoka kuutumia uwanja wa CCM LITI kama uwanja wake wa nyumbani na kuhamia
kwenye uwanja wao huo mpya



